Sunday, August 8, 2010

Waraka wa EPA

Lengo la nyaraka hii ni kutoa ufafanuzi wa kina kuhusu hoja mbalimbali

zilizojitokeza kutokana na ‘Hoja yangu ya Kuundwa kwa Kamati Teule ya

Bunge’, kuchunguza matumizi mabaya fedha za umma, uwezekano wa uwepo wa

ubadhirifu, uwizi na ufisadi mkubwa ndani ya BOT ambacho ni kioo cha

uchumi wa nchi yetu, kama ilivyo kwa Benki kuu yeyote duniani. Katika

Mkutano wa Hadhara uliofanyika Jangani tarehe 18 August, 2007 nilitoa

hadi tarehe 15 Septemba kwa Serikali kuchukua hatua mahususi dhidi ya

wahusika. Nilitoa tarehe hiyo makusudi. Leo nina nia ya kutoa ufafanuzi

wa kina zaidi, katika maeneo machache tu katika Tuhuma hizo ili

Watanzania walio wengi waelewe hasa ni nini kilichonisababisha kudai

kuundwa kwa Kamati Teule ya Bunge.

1. Utangulizi:

Kwa kifupi nilitoa Tuhuma nzito dhidi ya BOT na watendaji wake wakuu

ndani ya Bunge letu Tukufu, tarehe 25 June, 2007 wakati wa mjadala wa

Hotuba ya Bajeti ya Waziri Mkuu. Jioni hiyo hiyo, wakati wa mafungu kwa

mujibu wa Kanuni ya Bunge ya 104(1)(2) nikatoa Taarifa ya nia yangu ya

kuundwa kwa Kamati Teule ya Bunge.

Tarehe 26 June, 2007 kwa mujibu wa Kanuni hiyo nikawasilisha kwa Katibu

wa Bunge Barua yangu ya Taarifa ya nia hiyo kwa mujibu wa Matakwa ya

Kifungu cha 104(2) ya Kanuni iliyotajwa. Tarehe 8 Julai, baada ya

utafiti wa kina, nikawasilisha kwa Katibu wa Bunge ‘Maelezo yangu ya

Hoja ya Kuundwa kwa Kamati Teule ya Bunge’. Tarehe 13 August, 2007,

mchana nikapokea Barua kutoka kwa Mhe. Spika, yenye Kumb.na

CA.150/277/01/07 ikinitaka niwasilishe ‘vielelezo halisi’ ili yeye

‘akiridhika’ apange muda wa Hoja yangu kuingia Bungeni. Jioni hiyo hiyo

ya tarehe 13 Agosti, 2007 nikawasilisha kwa barua rasmi vielelezo vyote,

vikiwa katika Volumes (lV). Barua yangu iliorodhesha Vielelezo (a) to

(s).

Tarehe 15 Asubuhi, raia mwema, kutoka Usalama wa Taifa, akaniletea

waraka wa kuaminika kuaminika kutoka ndani ya Idara hiyo. Ushauri

uliotolewa baada ya kuchambua mambo mbalimbali unasomeka ifuatavyo:- “

Taarifa ya ukaguzi wa mahesabu ya benki Kuu ilipaswa kuwa siri na

haijulikani ni vipi imeweza kuvuja na kuwafikia wapinzani. Suala hili

likifikishwa bungeni linaweza kuwa na athari mbaya kwa serikali, hasa

kwa kuzingatia kuwa ni vigumu kupata majibu ya hoja hizi za CAG

yanayotosheleza. Ni vema Waziri Mkuu ajulishwe ili itafutwe njia ya

kuzuia hoja hii kuwasilishwa Bungeni. Idara inaendelea kuchunguza chanzo

cha uvujaji wa taarifa hiyo”

Nilitafakari sana hoja hii. Katika akili ya kawaida, ilionenakana

taarifa hii ni ya kweli. Mazingira yaliyojitokeza tarehe 13 Agosti,

ambapo Kamati ya Uongozi ya Wabunge wa CCM, ikiwa ni wajumbe wote wa

Kamati Kuu ya CCM walioko Bungeni, akiwemo na Spika ilikaa toka saa 5

hadi saa nane kwenye ukumbi wa Spika. Taarifa inayoaminika inasema kuwa

ajenda kuu ilikuwa hoja ya Mhe. Zitto Kabwe, na Hoja ya Dr. Slaa, zote

zikitaka kuundwa kwa Kamati Teule ya Bunge. Kuhusu Hoja yangu

“Maelekezo” mawili inaelekea yaliyotolewa na kikao hicho. Moja ni Spika

kuniandikia na kudai apetiwe ‘vielelezo Halisi’ ili ajiridhishe yeye

kabla ya hoja kuingia Bungeni, na pili, Hoja hiyo isipangiwe katika

Shughuli za Bunge (Order Paper) katika Mkutano huu yaani Mkutano wa Nane

wa Bunge. Hapo nikajiridhisha kuwa ushauri aliopelekewa Waziri Mkuu ndio

unatekelezwa. Na hivyo, nikajua kuwa i)Hoja haitaingizwa Bungeni safari

hii, ina inawezekana isipangiwe kabisa hata kikao kijacho,

ii) Ucheleweshaji wowote, unaweza kuathiri uchunguzi unaotakiwa, kwani

katika Tuhuma yeyote, hatua za haraka ni muhimu ili kusiwe na nafasi

yeyote ya kuingilia uchunguzi.

Kwa vile tuhuma ni nyingi sana, kwa leo naomba niwape mwanga kwenye

maeneo machache tu kama ifuatavyo:

2: TUHUMA ZA MSINGI ZA UBADHIRIFU NDANI YA BOT:

1: BENKI KUU KULIPA DENI LA MERREMETA CO.LTD LA TSHS Bilioni 155 KINYUME

NA

UTARATIBU:

Hapa kuna mambo ya msingi kadhaa Watanzania wanatakiwa kufahamishwa.

Kwa muda wa kama miaka mine sasa Wabunge wa Kambi ya Upinzani tumeihoji

Serikali itueleze

a) Meremeta Co.Ltd. ni mali ya nani na imeandikishwa wapi?

b) Mahesabu ya Kampuni hii yanatolewa kwanani

c) Tanzania inafaidika nini kutokana na Kampuni hii ambayo ilikabidhiwa

Mgodi wa dhahabu wa Buhemba, Mkoani Mara.

Miaka yote, pamoja na kuhoji Serikali ilishindwa kutoa majibu ya

kuridhisha, licha ya kusema tu Meremeta ni Kampuni ya Serikali, na

inaendeshwa na JWTZ, kwa lengo la kuisaidia kikosi chetu cha NYUMBU.

Majibu haya yako kwenye Hansard. Maswali mengine yote hayakujibiwa.

Mwaka jana, baada ya kuibana Serikali ilikiri kuwa Kampuni hii iko

kwenye hatua ya ‘Kufilisiwa’(Liquidation”) Majibu haya ya Serikali

yalileta mashaka makubwa sana. Ndipo ilipokuja nia ya kuundwa kwa Kamati

Teule kupata ukweli na majibu sahihi ya masuali hayo. Sasa basi Utafiti

wangu umeonyesha nini:

a) Meremeta Co.Ltd, tuliyoambiwa ni Kampuni ya Serikali, iliandikishwa

nchini Uingereza kama ‘Offshore Co.’ kwa hati ya Usajili na 3424504 kama

Private Ltd Co., iliyotolewa London, na Ofisi ya Msajili wa Makampuni,

Tarehe 19 August, 1997. Tarehe 3 Oktoba, 1997 Kampuni hiyo ikapata ‘Hati

ya Kutimiza Masharti’ yaani ‘Certificate of Compliance Na 32755.. utafiti

huu unaonyesha kuwa Tanzania inazo hisa 50% katika Kampuni hiyo na Share

mwingine ni Kampuni ya Afrika ya Kusini inayoitwa Triennex Co.Ltd nayo

yenye hisa 50%. Uchunguzi wa ziada unaonyesha Kampuni 2 zaidi zina hisa

moja moja nazo ni London Law Society Ltd (Hisa 1) na London Law

Secretarial Service Ltd yenye hisa moja. Hapa kuna utata mkubwa.

Meremeta ni ya nani? Meremeta ina hisa ngapi? Kama Meremeta

imeandikishwa kama Kampuni ya Kigeni Tanzania ni kwanini imepewa fedha

za Walipa kodi wa Tanzania? Na Iwapo Tanzania siyo peke yake yenye

katika umiliki wake, ni kwanini wakati wa ufilisi wake Benki Kuu ya

Tanzania kwa niaba ya Serikali yaTanzania ililipa Deni lote la Tshs 155,

Billioni, ambazo zilibadilishwa na kuwa Dola za Marekani

118,396460.36 na kuzipeleka kwenye akaunti isiyojulikana ya Nedbank Ltd

ya Afrika ya Kusini kupitia Benki ya HSB ya New York.Zingine

13,736,628.73 zililipwa Kampuni ya Tangold (nayo tutaieleza baadaye

kidogo) kwenye akaunti yake iliyoko Corporate Branch Dar-Es-Salaam. Hoja

hizi zilihitaji Kamati Teule kupata ufafanuzi wa Kina. Kwa kuwa

tumehujumiwa ni vema Watanzania wafahamu kilichoko ndani ya Benki yao

Kuu, na Serikali kwa ujumla wake.

b) Watanzania lazima wafahamishwe, Kampuni hii ilipata faida au hasara

kiasi gani. Taarifa ya Waziri wa Nishati na Madini inaeleza kuwa

Meremeta kwa mwaka 2006/7 imepata Tani 2.7 ya dhahabu. Mapato haya

yemeenda wapi? Utata huu unaelezwa vipi iwapo Serikali inaeleza kuwa

Kampuni ya Meremeta imefilisiwa na shughuli zake kuchukuliwa na TANGOLD

Ltd.

2: KAMPUNI YA TANGOLD LTD:

Bunge tukufu mara kadhaa limeelezwa kuwa Kampuni hii ni mali ya Serikali

ya Tanzania kwa asili mia moja. Hata hivyo utafiti wangu unaonyesha

kuwa;-

a) Kampuni ya TANGOLD Ltd, ni Kampuni ya Kigeni, iliyoandikishwa kwa

mara ya kwanza nchini Mauritius kwa hati ya usajili na. C 205006121

tarehe 8th April, 2005 na kupata Hati ya Kutimiza Masharti ( Certificate

of Complicance) na. 55661 ya 20th February, 2006 hapa Tanzania.

b) Memorandum and Articles of Association ya Kampuni hii, haionyeshi

popote kuwa ni mali ya Serikali wala kuwa ina uhusiano na Serikali.

c) Kifungu cha 7cha Articles hizo zinaonyesha kuwa Hisa zinaweza

kuhamishwa kwa Baba, mama, mtoto, mke, Babu na kadhalika wa wenye hisa

-Hapa kuna zuka utata mkubwa kabisa kuwa Je Serikali inao watu hao

wanaoweza kuhamishiwa Hisa?

d) Isitoshe, Mahesabu ya Kampuni hii iliyoanzishwa 2005 hayako popote?

Je ni kweli ilianzishwa ikakaa tu haikufanya Biashara? Ni kwanini

ilianzishwa ‘Offshore” na kama ilianzishwa kufanya Biashara imelipa kodi

kiasi gani ya Serikali.

e) Uchunguzi wa kina wa Hati zilizoko BRELA hazionyeshi popote kuwa

wakurugunzi wake, wanafanya kazi kwa niaba ya Serikali, kwani FORM zote

za Brela zinaonyesha tu Ukurugenzi au kazi zao kwingineko, lakini siyo

kuwa wanawakilisha Serikali kama Serikali.

f) Msajili wa Serikali ambaye kwa kawaida ni ndiye anayemiliki Mali zote

za Serikali kwa nia ya nchi si mojawapo wa Wakurugenzi.

g) Kampuni hii ndiyo iliyolipwa fedha tulizoona hapo juu? Fedha hizo ni

kwa ajili ya nini?

Je hapakuwa na haja nzito ya Bunge letu kufanya uchunguzi wa kina

kupitia Kamati yake Teule?

3: TUHUMA BOT KULIPA FEDHA KWA KAMPUNI

BINAFSI YA MWANANCHI GOLD CO.LTD.

Mwananchi Gold Co.Ltd. imeandikishwa nchini kama Kampuni Binafsi.

Katika mwaka wa Fedha wa 2004/2005 na 2006/2007 Kampuni hii imelipwa na

Benki kuu jumla ya Dola za Marekani zipatazo 5,512,398.55. Taarifa za

Ukaguzi zinaonyesha kuwa hadi 21 Decemba, Kampuni hii ilikuwa

imelimbikiza Riba ya Dola za Marekani 62,847.91, sawa na Tshs

78,753,459. Hii ni kwa sababu Kampuni hii ilitakiwa kulipa deni lake

ndani ya Miezi 6, na hadi tarehe hiyo ya ukaguzi, yaani miezi 18 baadaye

ilikuwa haijalipa hata senti moja.

Isitoshe, Deni la Dola za Marekani, 2,807,920, linaonekana kwa taarifa

ya ukaguzi kudhaminiwa (secured kwa dhahabu ghafi (raw gold)

iliyonunuliwa kwa fedha hizo hizo za mkopo. Yaani Watanzania tumekaangwa

kwa mafuta yetu wenyewe. Kwa taarifa za BRELA, Benki Kuu inahisa 500 tu

katika Kampuni hiyo, na NDC ina hisa 375. Kampuni ya Mwananchi Trust

Company Ltd ina hisa 1,123 na Chimera Co.ltd ina hisa 500. Kampuni

ilisajiliwa kwa Hati na.44962 ya tarehe 12 Desemba 2002 kama Private

Company, na kwa maana hiyo hairuhusiwi kuchukua fedha kutoka kwa Umma,

yaani kuuza hisa zake kwa Umma wa Tanzania. Kuna utata mkubwa sana

kuhusu hizo kumpanu nyingine za Chimera na Mwananchi Trust, lakini hayo

tuyazungumze wakati mwingine au katika masuali yenu. Taarifa za ukaguzi

zinaonyesha kuwa BOT imelipa pia fedha zifuatazo ambazo hazina maelezo:

Tarehe 17/7/2005 File 18003 Temp f/47 Dola za Marekani 95,000 kwa

Kampuni ya MGCL. Tarehe 29/0/7/2005 ‘Allowances’ dola 7,500 kwa kampuni

ya MGCL bila maelezo. Tarehe 18/01/2006 Transfer( Uhamisho) Tz Embassy,

Kinshasa, Dola za Marekani, 1,500,000.

Kwa chombo kikubwa kama BOT taarifa yeyote inayoacha wasiwasi haitakiwi

kabisa, kwani BOT ndio msimamizi wa Taasisi zote za Fedha, ndiyo

msimamizi wa Uchumi wa Tanzania nzima. Je, Hapakuwa na haja ya Kuundwa

kwa Kamati Teule ya Bunge iwapo Wakaguzi hawajapata hata nyaraka kujua

malipo haya yalikuwa ya nini?

4: TUHUMA ZA JUMLA:

Siku ya Hotuba ya Waziri Mkuu nilitaka pia kupata Ufahamisho kuhusu

taarifa zilizokuwepo katika vyombo vya Habari hasa Gazeti la Serikali

Daily News, Issue no. 0856-3812 na 9315 la 22 June, 2007 taarifa ambayo

haijakanashwa na Serikali hadi leo kuwa kuhusu Fedha zilizolipwa na BOT

kwa makampuni hewa, kiasi cha Tshs 30.8 Billion kupitia Kampuni wakala

ya Kagoda Agricultural Ltd. Sababu ya Mashaka katika malipo haya ni kuwa

Kampuni inasemekana ilisajiliwa Tarehe 29 Septemba, 2005, na ndani ya

majuma 8 ilikuwa imekwisha kupewa mkopo huu. Je, kwa akili ya kawaida,

jambo hili halileti utata wowote, na hapahitaji ukaguzi wa kina wa

Kamati Teule. Wakaguzi wa Serikali CAG hata baada ya utafiti wa kina

hakuweza kugundua Kampuni hizo, Italy, Ufaransa, Ujerumani, Japan na

wala USA. Kwa Taarifa yenu eneo hili pekee ndiyo Serikali ilikubali

kufanyiwa Uchunguzi wa kina na kinachoitwa na Serikali na ‘Forensic

Auditor’.

Kwa kuwa lengo la nyaraka hii ni kutoa picha kwa Watanzania kabla ya

hatua zaidi nitazochukua Tarehe 15 Septemba, nimeona nitoe haya machache

tu ili muyaelewe Hoja ya msingi, utata ulioko, na jinsi Serikali

inavyocheza Rasilimali na Mali ya Watanzania. Narudia kuwa suala hili

halina chembe ya Itikadi hata kidogo bali linaletwa kwenu kwa misingi ya

Uzalendo na mapenzi mema kwa nchi yetu tu.

Naomba kuwasilisha.

Wenu katika ujenzi wa Taifa letu,

Dr.Willibrod Peter Slaa,(MB)

MBUNGE WA KARATU.


1 comments:

Unknown said...

Safi sana! sikufananishi na baba wa taifa. ila angekuwepo leo angefurahi sana kuona kuna miongoni mwa vijana wanaofuata nyendo zake kuliko alio waaamini na hawakuaminika na matokeao yake kutufanya tuishi maisha ya dhiki ndani ya nchi tajiri

Post a Comment