Tuesday, October 26, 2010

kataeni kushawishiwa ama kuhusishwa katika fujo au vurugu-igp mwema.

NA MAGRETH KINABO – MAELEZO

MKUU wa Jeshi la Polisi nchini(IGP), Said Mwema amewaomba wananchi kuwa na ushirikiano katika kukataa kushawishiwa ama kuhusishwa katika uvumi, fujo au vurugu zozote zinazoweza kuingiza nchi kwenye machafuko yasiyo ya maana yoyote.

Aidha Mkuu huyo , amesema kuwa amani na usalama na utulivu hapa nchini vitadumishwa wakati wote kabla na baada ya uchaguzi, kwa kuhakikisha kwamba sheria , kanuni na taratibu za nchi zinafuatwa ipasavyo.

“Tukumbuke kwamba vitendo vyovyote vya uvunjwaji wa sheria, kabla na baada ya uchaguzi ni uhalifu.Sheria haina udhuru, inachukua mkondo wake mara moja endapo ukiukwaji umefanyika. Hivyo kutii sheria na taratibu za uchaguzi ni wajibu wa kila mpiga kura na kila mwananchi,” alisema Mwema.

Aliongeza kuwa baada ya kura kupigwa na zoezi hilo kufungwa rasmi, hatua inayofuata ni kuzichambua na kuzihesabu ili kupata matokeo, hivyo huo ndo wakati wananchi wanatakiwa kuwa na subira, kwa sababu zoezi hilo ni muhimu na linapaswa kuendeshwa kwa umakini wa hali ya juu ili, haki itendeke na kuepusha malalamiko.

Mkuu huyo alisema baada ya matokeo kutangazwa ni muhimu kutambua kwamba aliyeshinda ndiye aliyepigiwa kura nyingi na watu wengi.

“Wote tunawajibu wa kumkubali , kumtambua na kushirikiana naye ili kumsaidia kutimiza wajibu wake kama kiongozi wa watu wote,” alisema.

Naye Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Mbarouk Abdulwakil aliwataka wananchi wote bila kujali itikadi au udini kuendelea kuwa na msukumo wa utaifa na kuacha maslahi binafsi ili amani, usalama na utulivu vidumu kabla ya baada ya uchaguzi.

Alisema wizara yake inawahakikishia wananchi kwamba nchi itakuwa katika hali ya amani, usalama na utulivu wakati wote huku, hivyo alisisitiza ushirikiano kutoka kwa wananchi .

0 comments:

Post a Comment