Thursday, February 17, 2011

Tamko la CHADEMA kuhusu Mabomu ya Gongo la Mboto

MAAFA YA GONGO LA MBOTO: WAZIRI WA ULINZI NA MKUU WA MAJESHI WAJIBIKE!

TAARIFA KWA UMMA
DODOMA, FEBRUARI 17, 2011

Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni inayoongozwa na Chama cha Demokrasia na
Maendeleo (CHADEMA) imeeleza kushtushwa na kusikitishwa na taarifa za
milipuko ya mabomu katika Ghala la Kuhifadhi Silaha la Kambi ya Jeshi la
Wananchi wa Tanzania (JWTZ) katika eneo la Gongo la Mboto, Dar es Salaam
jana jioni.

Aidha, kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni imewapa pole ndugu, jamaa, marafiki
na wananchi wote wa Tanzania kwa sababu ya maafa haya. Pia Kambi hiyo
imezitaka mamlaka zote za umma zinazohusika kuchukua hatua za haraka
kuhakikisha wananchi wote walioathirika na maafa haya wanapatiwa huduma zote
wanazohitaji katika kipindi hiki cha msiba huu. Hii ni pamoja na kuwapatia
huduma za maziko wale wote waliofariki, matibabu kwa waliojeruhiwa na
hifadhi kwa wale waliopoteza makazi yao. Aidha, ni muhimu kwa vyombo vya
usalama kuhakikisha ulinzi wa mali za wananchi katika maeneo yote
yaliyoathirika na ambazo zitakuwa hazina ulinzi baada ya wananchi kukimbia
maeneo yao.

Taarifa ya Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni imeeleza kwamba tukio hili ni la
kushtusha na kusikitisha hasa kwa kuzingatia kwamba haijapita miaka miwili
tangu tukio la aina hiyo hiyo litokee katika Ghala ya Silaha ya Kambi
nyingine ya JWTZ katika eneo la Mbagala, Dar es Salaam, ambalo lilisababisha
vifo vya zaidi ya watu thelathini na uharibifu mkubwa wa mali za umma na za
wananchi binafsi. Aidha, milipuko ya Mbagala ilipelekea Serikali kutumia
mabilioni ya fedha za umma kwa ajili ya malipo ya fidia kutokana na vifo,
majeruhi na uharibifu wa mali binafsi za wananchi.

Akielezea tukio la milipuko ya Gongo la Mboto, Msemaji wa Ulinzi wa Kambi
Rasmi ya Upinzani Bungeni, Mh. Joseph Selasini alisema: “Milipuko ya Gongo
la Mboto inaonyesha dhahiri kwamba Serikali ya Awamu ya Nne ya Chama cha
Mapinduzi (CCM) haijajifunza lolote kutokana na maafa yaliyotokea Mbagala
mwaka juzi. Maana kama Serikali ingejifunza kutokana na maafa hayo
ingeshachukua hatua za dharura na za haraka kuhakikisha kwamba maafa ya aina
hii hayatokei tena.” Mh. Selasini alizitaja baadhi ya hatua hizo kama ni
pamoja na kuhamisha maghala yote ya silaha na mabomu yaliyo karibu na maeneo
wanayoishi raia na kuyapeleka katika Kambi za JWTZ zilizoko mbali kabisa na
maeneo ya raia. “Haiwezekani kwa Serikali kuendelea kuweka maghala ya silaha
katika Kambi za Jeshi zilizo karibu na wananchi na hivyo kuhatarisha maisha
yao namna hii”, alisema Mh. Selasini.

Aidha, Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni imewataka Waziri wa Ulinzi na Jeshi
la Kujenga Taifa Dr. Hussein Mwinyi na Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi Jenerali
Davis Mwamunyange kujiuzulu mara moja ili kuwajibika kisiasa kutokana na
maafa ya Gongo la Mboto na ili kupisha uchunguzi huru na wa kina wa chanzo
na/au sababu za milipuko hiyo. Mh. Selasini alisema: “Dr. Hussein Mwinyi
alikuwa Waziri wa Ulinzi wakati wa maafa ya Mbagala; na Jenerali Mwamunyange
alikuwa Mkuu wa Majeshi. Maafa ya Mbagala yalitokea chini ya dhamana na/au
usimamizi wao. Na mara baada ya maafa hayo, Waziri Mwinyi na Jenerali
Mwamunyange waliliahidi taifa kwamba maafa ya aina hii hayatatokea tena.
Sasa yametokea. Inaelekea, kwa hiyo, kwamba ahadi yao ilikuwa sio ya kweli
na/au hawakuhakikisha kwamba inafanyiwa kazi ili iwe ya kweli. Viongozi hawa
hawana budi kuwajibika kwa hiari yao wenyewe au kuwajibishwa kama
itahitajika.”

Mh. Selasini aliongeza kusema kwamba hadi leo hakuna taarifa yoyote rasmi
iliyowahi kutolewa hadharani kwa wananchi na/au kwa wawakilishi wao Bungeni
ya chanzo na/au sababu za maafa hayo. “Hadi leo hii wananchi na/au
wawakilishi wao Bungeni hawajaambiwa kama kulikuwa na makosa ya makusudi
na/au ya uzembe na/au kama hatua zozote za kinidhamu na/au za kisheria
zilizochukuliwa dhidi ya mtu yeyote kutokana na kusababisha na/au kuwajibika
kwa maafa hayo. Jana maafa mengine ya aina hiyo hiyo yametokea tena na kwa
kadri ya taarifa rasmi ya Serikali watu wengi wameuawa na wengi wengine
kujeruhiwa na mali nyingi kuharibiwa. Kwa sababu hizo, huu ni wakati muafaka
kwa Dr. Mwinyi na Jenerali Mwamunyange kuonyesha uadilifu wao kwa kujiuzulu
nafasi zao ili kuwajibika kwa maafa haya.”

Mwisho, Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni imependekeza iundwe Tume Huru ya
Uchunguzi na/au Kamati Teule ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ili
kuchunguza kwa kina chanzo, sababu na madhara yote yaliyosababishwa na
milipuko ya Gongo la Mboto. “Kwa kuzingatia historia ya uchunguzi wa
milipuko iliyotokea Mbagala mwezi Aprili 2009, Tume Huru na/au Kamati Teule
ya Bunge lazima itoe taarifa yake hadharani kwa kupitia Bunge la Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania”, alishauri Mh. Selasini.

0 comments:

Post a Comment